Kitaifa, Kimataifa, Siasa, Michezo na Burudani

CCM, Chadema kuchuana uchaguzi wa ubunge Januari 2018 .

Image result for tume ya Taifa ya uchaguzi

NA MWAMDISHI WETU
WAKATI vumbi la kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mdogo wa Madiwani katika kata 43 za mikoa 19 ya Tanzania Bara, likiwa halijatulia, vumbi jingine la uchaguzi mdogo linatarajiwa kutimka mapema mwezi ujao katika majimbo matatu ya ubunge na kata sita.
Novemba 26, mwaka huu, kulifanyika Uchaguzi Mdogo wa Madiwani katika kata 43 za mikoa 19 ya Tanzania Bara, ambao ulishuhudia Chama Cha Mapinduzi (CCM) kikizoa kata 42 kati ya hizo na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), katika uchaguzi uliokuwa na mtifuano mkubwa.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) jana ilitangaza kuwa Januari 13, mwakani kutafanyika Uchaguzi Mdogo katika majimbo ya Longido katika Halmashauri ya Wilaya ya Longido mkoani Arusha, Songea Mjini katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma na Singida Kaskazini katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida mkoani Singida.
NEC imezitaja kata ambazo ziko wazi kuwa ni Kimandolu (Halmashauri ya Jiji la Arusha), Kihesa (Halmashauri ya Manispaa ya Iringa), Bukumbi (Halmashauri ya Wilaya ya Uyui), Kurui (Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe), Keza (Halmashauri ya Wilaya ya Ngara) na Kwagunda (Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe).
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Makamu Mwenyekiti wa NEC, Jaji Mkuu mstaafu Zanzibar, Hamid Mahmoud Hamid alisema walipokea barua kutoka kwa Spika wa Bunge kuhusu kuwapo kwa nafasi wazi za majimbo ya uchaguzi ya Singida Kaskazini Mkoa wa Singida kuanzia Oktoba 30, mwaka huu.
Alieleza kuwa hiyo ilitokana na aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, Lazaro Nyalandu, kuvuliwa uanachama na CCM, hivyo kwa mujibu wa Ibara ya 71(1)(f) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, alipoteza sifa ya kuwa mbunge.
Ibara hiyo inaeleza kuwa “Mbunge atakoma kuwa Mbunge na ataacha kiti chake katika Bunge – iwapo Mbunge ataacha kuwa mwanachama wa chama alichokuwamo wakati alipochaguliwa au alipoteuliwa kuwa Mbunge”.
Alisema kuwa Jimbo la Uchaguzi la Songea Mjini mkoani Ruvuma, liko wazi kuanzia tarehe 24 Novemba, 2017 kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo, Ndugu Leonidas Tutubert Gama.
“Aidha, kwa mujibu wa kifungu cha 113(1)(2) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi Sura ya 343, Tume imepokea Hati kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, ikithibitisha kuwa Jimbo la Longido Mkoa wa Arusha lipo wazi kuanzia tarehe 30 Oktoba 2017 kufuatia Mahakama Kuu kufuta matokeo ya uchaguzi wa jimbo hilo na hivyo Ndugu Onesmo Ole Nangole aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo kupoteza sifa za kuwa Mbunge,” alieleza Jaji Mkuu mstaafu Hamid.
Akielezea taratibu za mchakato huo wa uchaguzi, Makamu Mwenyekiti wa NEC alisema fomu za uteuzi katika majimbo ya Singida Kaskazini na Longido na kata za Keza, Kimandolu, Kwagunda, Bukumbi, Kurui na Kihesa, zitatolewa kati ya Desemba 12 hadi 18, mwaka huu.
Kwa Jimbo la Songea Mjini, fomu za uteuzi itakuwa kati ya Desemba 14 hadi Desemba 20, mwaka huu. Kuhusu uteuzi, alisema wagombea katika majimbo ya Singida Kaskazini na Longido na kata za Keza, Kimandolu, Kwagunda, Bukumbi, Kurui na Kihesa, utafanyika Desemba 18, mwaka huu; wakati kwa Jimbo la Songea Mjini itakuwa Desemba 20, mwaka huu.
Aidha, taarifa hiyo ya NEC ilieleza kuwa kampeni za Uchaguzi Mdogo katika majimbo ya Singida Kaskazini na Longido na kata za Keza, Kimandolu, Kwagunda, Bukumbi, Kurui na Kihesa zitaanza Desemba 19, mwaka huu na kumalizika Januari 12, 2018.
Ilieleza kuwa kampeni za Uchaguzi Mdogo katika Jimbo la Songea Mjini, zitaanza Desemba 21, mwaka huu na kumalizika Januari 12, 2018, siku moja kabla ya uchaguzi katika majimbo hayo matatu na kata sita.
“Tunavikumbusha vyama vya siasa na wadau wote wa uchaguzi wazingatie Sheria, Kanuni, Taratibu, Miongozo na maelekezo yote wakati wa kipindi cha Uchaguzi Mdogo wa majimbo matatu na kata sita,” ilieleza NEC.

Kata 43 zilizofanya uchaguzi wa madiwani hivi karibuni na majina ya mikoa kwenye mabano ni: Murieti, Moita, Musa, Ambureni, Ngabobo, Maroroni, Leguruki na Makiba (Arusha), Mbweni, Kijichi na Saranga (Dar es Salaam), Chipogolo (Dodoma), Bukwimba na Senga (Geita), Kitwiru na Kimala (Iringa), Bomambuzi, Mnadani, Machame Magharibi na Weruweru (Kilimanjaro), Chikonji na Mnacho (Lindi), Nangwa (Manyara), Ibighi(Mbeya), Kiroka na Sofi (Morogoro), Milongodi, Reli na Chanikanguo (Mtwara), Kijima na Mhandu (Mwanza), Sumbawanga (Rukwa), Lukumbule, Kalulu na Muongozi (Ruvuma), Siuyu (Singida), Nyabubinza(Simiyu), Ndalambo (Songwe), Nata na Muungano (Tabora) na Majengo, Lukuza na Mamba (Tanga). Mbali na CCM na Chadema, vyama vingine vinavyotarajiwa kusimamisha wagombea ubunge na udiwani ni pamoja na Chama cha Wananchi (CUF), NCCRMageuzi, ACT-Wazalendo, UDP na UPDP.
Labels:

Post a Comment

[facebook]

MKRdezign

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget