Kitaifa, Kimataifa, Siasa, Michezo na Burudani

September 2017

1
Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo (wapili kulia), akimkabidhi Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Simon Sirro (katikati), mchoro wa ramani ya nyumba za Polisi za kisasa zitakazojengwa kufuatia za awali kuteketea kwa moto. Hatua ya ujenzi imeanza mara moja kufuatia Mhe. Rais Dkt. John Magufuli, kutoa kiasi cha shilingi milioni 260 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba hizo. Wa pili kushoto ni Mwenyekiti wa Makampuni ya Hanspaul, Kamaljit Singh, na kulia ni Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha (DCP) Charles Mkumbo na wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi wa Wakala ya Majengo Arusha Bw. Victor,.
2
Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Simon Sirro, akiagana na Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo, alipomtembelea ofisini leo tayari kwa safari ya kurejea Dar es salaam, baada ya kuwapapole na  kukagua eneo la nyumba za Polisi zilizoteketea kwa moto.
Picha na Jeshi la Polisi.

korosho
Na Mwamvua Mwinyi,Pwani
MKUU wa mkoa wa Pwani,mhandisi Evarist Ndikilo,amekemea biashara ya korosho kufanywa katika mfumo wa kangomba na Chibuda,ambao huwakandamiza wakulima wa zao hilo.
Amesema korosho zote zitakazokutwa kwenye magari yatakayokamatwa yakiwa kwenye mifumo isiyo rasmi badala ya stakabadhi ghalani ambao unatambulika ,korosho zitataifishwa  na mtuhumiwa atakamatwa na jeshi la polisi.
Akizungumzia juu ya zao la biashara la kimkakati mkoani hapo,mhandisi Ndikilo,alieleza kwamba mbali ya kutaifisha korosho pia mtuhumiwa atatakiwa kutoa faini .
Alisema wakulima wa korosho wasikubali kurubuniwa na madalali ama wanunuzi wachache ambao hutumia jasho lao kujinufaisha .
Mkuu huyo wa mkoa ,alielezea kuwa,anaedhani atatengeneza fedha kwa kutumia mifumo hiyo amechelewa kwani msimu huu hatotaka kuona mkulima wa korosho anakandamizwa kimaslahi .
Mhandisi Ndikilo,alitoa wito kwa wakulima kuunga mkono uhamasishaji wa mfumo wa stakabadhi ghalani  ili kuongeza tija na kasi ya kukuza zao hilo la kimkakati mkoani humo.
“Mfumo huu unarahisisha upatikanaji wa takwimu sahihi za korosho kwa ajili ya kupanga mipango ya maendeleo ya tasnia ya korosho huku ukipunguza wimbi la madadali wanaonunua korosho na kutorosha kwa njia ya magendo”alisema mhandisi Ndikilo.
Alisema mfumo wa stakabadhi ghalani hukusanya mazao kwenye ghala maalum lililosajiliwa na serikali kwa lengo la kuyauza kwa bei ya ushindani,na kumkomboa mkulima wa korosho.
Mhandisi Ndikilo,alisema mwaka 2015-2016 wakulima waliweza kuuza korosho zao grade ya kwanza sh.2,900 kwa kilo ,hivyo wanatarajia msimu huu korosho nyingi zitauzwa kwa bei nzuri na kutopata changamoto zinazokuwa zikiwakabili wakati wa soko.
Aidha aliwataka wataalamu wa zao la korosho kusimamia wakulima hao kupanda miche mipya ya mikorosho.
Baadhi ya wakulima katika wilaya ya Kibiti na Rufuji ,waliomba serikali ya mkoa huo kuendelea kuwapigania katika changamoto mbalimbali zinazojitokeza mara kwa mara hasa wakati wa kuuza korosho zao.
Walisema kumekuwa na tabia kwa baadhi ya makampuni yanayonunua korosho zao ,kuchelewesha malipo ,ama kuweka dosari ambazo huwakatisha tamaa .
Mikoa ya Ruvuma na Pwani ilianza kutumia mfumo wa stakabadhi ghalani katika msimu wa mwaka 2009/2010 kwa lengo la kumuinua mkulima wa zao hilo.

Kibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Mpoki Ulisubisya akiongea na waandishi wa habari (Hawapo kwenye picha) mapema leo jijini Dar es salaam wakati wa tukio la kupokea mashine ya kutoa dawa ya usingizi kutoka kwa taasisi ya Utepe mweupe, pembeni ni Waziri  wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mh. Ummy Mwalimu.
#2
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mh. Ummy Mwalimu akipokea msaada wa mashine ya kutoa dawa ya usingizi  kutoka kwa Mratibu wa Utepe Mweupe Bi.Rose Mlai wakati wa  tukio lililofanyika mapema leo katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es salaam.
#3
Picha ya pamoja ikiongozwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mh. Ummy Mwalimu wakati wa tukio la kupokea mashine ya kutoa dawa ya usingizi kutoka kwa taasisi ya Utepe mweupe lililofanyika mapema leo katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es salaam.
#4
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mh. Ummy Mwalimu akiongea na waandishi wa habari (hawapo kwenye picha) wakati wa kupokea msaada wa mashine ya kutoa dawa ya usingizi kutoka kwa taasisi ya Utepe mweupe mapema leo jijini Dar es salaam, pembeni ni Mratibu wa Utepe Mweupe Bi.Rose Mlai.
#5
Mashine ya kutoa dawa ya usingizi (Anesthesia) iliyokabidhiwa kwa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto  mapema leo jijini Dar es salaam  kutoka kwa  taasisi ya Utepe Mweupe chini ya Mratibu wake Bi.Rose Mlai.
…………………….
NA WAMJW-DAR ES SALAAM
SERIKALI kupitia Wizara ya Afya,Maendeleo ya jamii,Jinsia, Wazee na Watoto imejidhatiti kujenga vyumba vya upasuaji 170 kwa wajawazito ili kupunguza vifo vya mama wajawazito na watoto wachanga mpaka kufikia Juni 2018.
Akizungumza hayo wakati wa kupokea mashine ya kutoa dawa ya usingizi Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia ,Wazee na Watoto Ummy Mwalimu alisema kuwa ujenzi wa vyumba hivyo vitasaidia kupunguza vifo vya wajawazito kwa asilimia 80  kufika 2025.
“ Si tu vyumba vya upasuaji bali tutaimarisha mahitaji muhimu ikiwemo kujenga maabara ya damu,wadi za wazazi,tutanunua vifaa vyote vya upasuaji na kujenga nyumba moja ya watumishi wa afya kwenye kila kituoa cha kutolea huduma ya afya” alisema Waziri Ummy.
Mbali na hayo Waziri Ummy amesema kuwa msaada wa mashine hiyo ya kutoa dawa ya usingizi kutoka  Utepe Mweupe utaisaidia kupambana  kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wachanga kwa asilimia 40 kufikia 2020 nchini.
Aidha Waziri Ummy amemuagiza Katibu Mkuu Wizara ya afya kuongeza wataalamu wa kutoa dawa ya usingizi wakati Serikali ipo katika mkakati wa kuongeza vifaa na dawa kwenye vituo vinavyotolea huduma ya afya hasa uzazi.
“Kama mpaka Juni mwakani tutakuwa tumemaliza hivyo Vyumba 170 vya upasuaji  wa kutoa watoto kwa wajawazito basi Katibu Mkuu na watendaji wako  mnatakiwa kuongeza wataalamu wa kutolea dawa ya usingizi wawili kila kituo kwa hiyo jumla wawe wataalamu 340” alisisitiza Waziri Ummy.
Kwa mujibu wa Waziri Ummy amesema kuwa Serikali imejiongeza kwa kutenga bilioni 8 kwa ajili kununua dawa za uzazi salama  ikiwemo dawa za kuzuia kifafa cha mimba,kuzuia mama kuvuja damu na hupatikana bila ya gharama yoyote.
Mbali na hayo Waziri Ummy amewataka wanawake  kuhudhuria kliniki angalau mara nne kwa mwaka ili kuweza kutambua hali na usalama wa ujauzito na kiumbe kiliochokuwa tumboni kabla ya kujifungua kwa dhumuni la kujifungua salama.
Kwa upande wake mratibu wa Taasisi ya Utepe mweupe Bi. Rose Mlai amesema kuwa mashine hiyo ya kutolea dawa ya usingizi imetolewa na Shirika la Gradians Health kutoka nchini Marekani kupitia Muungano wa Utepe mweupe wa uzazi salama ili kudumisha afya ya mama na mtoto.


Dar es Salaam,
Serikali imesitisha uchapishaji na usambazaji wa gazeti la kila wiki la RAIA MWEMA kwa muda wa siku 90 (miezi mitatu) kuanzia leo. Agizo hili pia linahusu toleo la mtandaoni. Adhabu hii inatokana na toleo na. 529 la tarehe 27 Septemba–3 Oktoba, 2017 lililochapisha habari ya uchambuzi inayosomeka “URAIS UTAMSHINDA JOHN MAGUFULI.”
Serikali inasisitiza uchambuzi huu ni maoni yao ya haki (fair comment), hata hivyo, kwa bahati mbaya, na nia ovu, makala hiyo ilisheheni nukuu za kutunga na zisizo za kweli zikimsingizia Rais John Pombe Magufuli. Gazeti hili pia limepata kuonywa huko nyuma kwa makosa mbalimbali.  
Nukuu za uongo, kutungwa na zenye nia mbaya zikidai Rais alipata kusema: “Suruali za zamani msizitupe, mtazihitaji baadae,” na “Watakaobaki  Dar es Salaam baada ya mwezi wa saba watakuwa wanaume kwelikweli.
Walipotakiwa kuthibitisha wapi iwe ndani au nje ya nchi Rais alipata kutoa kauli hizo, wahariri wa RAIA MWEMA waliomba muda, wakapewa. Wakarejea na kuthibitisha kuwa hawana ushahidi huo, wakakiri kosa na kuomba radhi.
Bado Serikali inaamini kwamba Watanzania tukiufanyia mzaha upotoshaji wa taarifa na uchochezi katika zama hizi za TEHAMA amani na utulivu tulivyojivunia kwa miaka mingi vitapotea na kukaribisha maafa kama ilivyotokea kwingineko duniani.
Serikali, katika uamuzi huu, uliochukuliwa kwa mujibu wa mamlaka aliyonayo Waziri wa Habari katika kifungu cha 59 cha Sheria ya Huduma za Habari Na. 12, 2016, imetoa adhabu ndogo tofauti na ukubwa wa kosa kwa kuwa wahariri wa gazeti hili hawakufanya tashtiti, wamekiri kosa.
Hata hivyo katika suala hili tunajifunza tena mambo kadhaa kuhusu changamoto za kiwango cha weledi wa uandishi wa habari nchini kiasi inatulazimu kutoa ufafanuzi wa kina kwa faida ya umma na tasnia yenyewe; kwamba uandishi ni taaluma adhimu na yenye haki na wajibu vinavyopaswa kufuatwa na si kufanyiwa dhihaka. 
Mintaarafu, mmoja wa wanasiasa waasisi wa Taifa la Marekani wanaotambulika kuwa waumini wakubwa wa uhuru wa habari, Thomas Jefferson, pamoja na kupigania sana uhuru huo, katika barua kwenda kwa rafiki yake, James Madison, wakati wa mjadala wa katiba mpya nchini humo alisisitiza wajibu wa vyombo vya habari hasa katika “….kutodhalilisha heshima ya mtu au kuharibu amani na utulivu….”
Kwa upande wake, John Stuart Mills, Muingereza anayetajwa kuwa “Baba wa Haki ya Kujieleza”ambaye katika kitabu chake mashuhuri cha “On Liberty” alitetea sana uhuru wa habari, naye alitambua umuhimu wa kutekeleza haki kwa kulinda haki za wengine alipoandika:
The only freedom which deserves the name is that of pursuing our own good in our own way, so long as we do not attempt to deprive others of theirs, or impede their efforts to obtain it.”
Aidha, Mahatma Gandhi, Baba wa Taifa la India na mpigania uhuru na haki asiyetiliwa shaka, naye aliamini katika uhuru wa habari lakini alionya vyombo vya habari lazima vitimize wajibu wao wa kutoandika uongo na uzushi aliposema:
I venture to suggest that rights that do not directly from duty well performed are not worth having…. The superficiality, the one-sidedness, the inaccuracy and often even dishonesty that have crept into modern journalism, continuously mislead honest men who want to see nothing but justice done.”
Mitazamo hii ya kifalsafa ya magalacha hawa mashuhuri duniani, imeenziwa na kutiliwa nguvu katika mikataba na sheria mbalimbali za kimataifa za haki za binadamu ambazo nchi yetu pia imeiridhia. Kifungu cha 19(3) cha Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kisiasa na Kiraia ambao Tanzania imeuridhia tangu mwaka 1976, kinasisitiza wajibu huu kikisema:
“3. The exercise of the rights provided for in paragraph 2 of this article carries with it special duties and responsibilities. It may therefore be subject to certain restrictions, but these shall only be such as are provided by law and are necessary:  (a) For respect of the rights or reputations of others;  (b) For the protection of national security or of public order (ordre public), or of public health or morals.
Vyombo vya habari nchini vinasisitizwa kuendelea kutekeleza wajibu huo. Serikali itaendelea kulinda uhuru wa habari unaosimama katika misingi iliyoainishwa katika nukuu hizi za wanafalsafa na sheria za kimataifa. Tunawatakia Bodi ya Wakurugenzi na wahariri wa gazeti la Raia Mwema utekelezaji mwema wa agizo hili. 
Imetolewa na:
Dkt. Hassan Abbasi,
Mkurugenzi, Idara ya Habari-MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikal

Pix 01
Mjumbe wa Sekretarieti toka Taasisi ya Ulingo wa Wanawake Bi. Saum Rashid akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wakitoa karipio juu udhalilishaji wa wanawake katika mitandao kwa kisingizio cha siasa, katikati ni Bi. Angelina Mutahiwa na kulia ni Bi. Dominata Rwechungura wajumbe wa Sekretarieti hiyo.
Pix 04
Baadhi ya waandishi wa Habari wakimsikiliza Mjumbe wa Sekretarieti toka Taasisi ya Ulingo wa Wanawake Bi. Angelina Mutahiwa (aliyekaa katikati) wakati wakitoa karipio juu udhalilishaji wa wanawake katika mitandao kwa kisingizio cha siasa.
Pix 02
Mjumbe wa Sekretarieti toka Taasisi ya Ulingo wa Wanawake Bi. Angelina Mutahiwa akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wakitoa karipio juu udhalilishaji wa wanawake katika mitandao kwa kisingizio cha siasa, kushoto ni Bi. Saum Rashid na kulia Bi. Dominata Rwechungura wajumbe wa Sekretarieti hiyo.
Pix 03
Mjumbe wa Sekretarieti toka Taasisi ya Ulingo wa Wanawake Bi. Angelina Mutahiwa akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wakitoa karipio juu udhalilishaji wa wanawake katika mitandao kwa kisingizio cha siasa, kushoto ni Bi. Saum Rashid na kulia Bi. Dominata Rwechungura wajumbe wa Sekretarieti hiyo.
Picha na Eliphace Marwa – Maelezo
………………..
Na Thobias Robert- MAELEZO
29-09-2017
Taasisi isiyo ya kiserikali inayoundwa na Jumuiya za Wanawake wa Vyama vyote vya siasa (Ulingo) imelaani vitendo vya matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii vinavyofanywa na baadhi ya watu dhidi ya viongozi wanawake wana siasa pamoja na serikali kwa ujumla.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Mjumbe wa Sekretarieti ya Ulingo Saum Rashid alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kwaaajili ya kulaani watu wanaotumia mitandao ya kijamii kuwadhalilisha na kuwavunjia heshima viongozi wanawake.
“Matusi ambayo wanatupiwa na watu wasio na maadili ni matusi siyo kwa wahusika tu bali kwa wanawake wote, hivyo ikumbukwe kuwa hao wanaowalenga wanafamilia, watoto na marafiki na wanaongoza mamilioni ya watanzania,” alifafanua Bi. Saum.
Akizungumza bila kuwataja wanaotumia vibaya mitandao ya kijamii kudhalilisha viongozi, Bi.Saum alisema wanawake wanapodhalilishwa hasa na wanawake wenzao inawakatisha tamaa katika kutimiza majukumu yao hivyo akaomba mamlaka husika kusimamia Sheria ili mitandao isitumike vibaya.
Aidha Bi. Saum amesema kuwa anaamini viongozi wanawake ambao wamepewa heshima na dhamana ya kuongoza, wana uwezo mkubwa na wanastahili kuwa kwenye nafasi walizo nazo .
Taasisi hiyo ambayo inawashirikisha pia watu wenye ulemavu imelaani vikali vitendo vya udhalilishaji na kuwataka watanzania warejee kwenye misingi ya utu na kuthaminiana kama maadili ya kitanzania yanavyoelekeza hasa kwa watoto wa kike.
Kwa upande wake Angelina Mutahiwa ambaye pia ni Mjumbe wa taasisi ya Ulingo alisema kuwa, mwanamke ni mlezi mzuri wa maadili katika jamii hivyo kumdhalilisha ni kuvunja malezi na maadili katika jamii na kuchochea vitendo viovu dhidi yake ambavyo vitadumu kizazi hadi kizazi.
 “Wale wachache ambao wameonesha utovu wa nidhamu kwa kuendelea kumnyanyasa mwanamke watambue kwamba wao hawapo juu ya sheria na katiba ya nchi iko wazi hairuhusu mwanamke kudhalilishwa, kuonewa wala kufanyiwa vitendo vya kikatili haikubaliki na hatutakubali,” alisistiza  Bi.Mutahiwa.
Ulingo ni taasisi isiyo ya kiserikali inayoundwa na jumuiya za wanawake wa vyama vyote vya siasa vilivyosajiliwa kwenye na Msajili wa vyama vya siasa hapa nchini kwa lengo la kuwajengea uwezo wanawake katika nyanja mmbalimbali ili waingie kwenye vyombo vya maamuzi.
Taasisi hiyo kwa sasa inapigania haki sawa kwa wanawake yaani 50/50 kwani waaamini kuwa uongozi ni haki ya kila mtu kwa maana ya wanawake na wanaume.

MAHAKAMA  ya Hakimu Mkazi Kisutu imeamuru kwa mara nyingine mshtakiwa Harbinder Sethi akatibiwe katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ndani ya siku 14.
Korti imesema iwapo hilo halitatekelezwa, mkuu wa gereza afike mahakamani kujieleza. Sethi yupo mahabusu katika Gereza la Segerea.

Amri hiyo ya mahakama imetolewa baada ya Wakili wa Serikali Mwandamizi, Kishenyi Mutalemwa kudai kesi ilipangwa leo Ijumaa kwa ajili ya kutajwa na upelelezi haujakamilika, hivyo aliomba shauri lipangiwe tarehe nyingine ya kutajwa.

Baada ya maelezo hayo, wakili Joseph Makandege anayemwakilisha Sethi alieleza kuwa kumekuwepo mfululizo wa amri za Mahakama zikiagiza mteja wake akapatiwe matibabu na kufanyiwa uchunguzi Muhimbili.
“Hadi leo asubuhi tuliwasiliana na mteja wetu na kubaini hajapelekwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kama amri za Mahakama zilivyoagiza, hivyo ni rai yetu kwamba kitendo hicho cha kutotekelezwa amri za Mahakama ni ukaidi wa amri halali za Mahakama yako tukufu,” amesema Makandege.


Amesema kwa kuwa upande wa mashtaka umekaidi amri za Mahakama, anaomba itoe adhabu inayostahili.

Makandege amesema kitendo cha upande wa mashtaka cha kutotekeleza amri za Mahakama kinasigana na kukiuka mamlaka aliyopewa Mkurugenzi wa Mashtaka .

“Mkurugenzi wa Mashtaka katika kutekeleza majukumu yake anapaswa kuongozwa na kutenda haki, lengo ni kutogeuza mashtaka ya jinai na mahakama kuwa ni vyombo vya utesaji,” amesema.

Ameomba Mahakama itoe adhabu stahiki kwa kuwa hilo linaonyesha dhahiri kuwa mashtaka yaliyopo ni ya hila yenye lengo la kuwaadhibu washtakiwa na hasa mshtakiwa wa kwanza Sethi kabla hawajahukumiwa.

Wakili Makandege ameiomba Mahakama iitupilie mbali hati ya mashtaka na kuwaachia huru washtakiwa ili Sethi apate wataalamu wa matibabu yake katika hospitali ikiwemo Muhimbili.

Mwendesha Mashtaka Mwandamizi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai amedai tatizo limeshajitokeza katika utekelezaji wa amri za Mahakama.

Swai amedai Magereza wamekuwa wakiwatibu wafungwa na mahabusu hata pasipokuwa na amri ya Mahakama.
Amesema kilichojitokeza ni utaratibu wa kumpeleka Sethi katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

“Tumejitahidi kuwasiliana na Magereza wapo katika hatua za mwisho, tunaomba muda wa ziada ili tuiwezeshe Magereza kukamilisha utaratibu wa kumpeleka Sethi Muhimbili, hatujakataa tunaomba muda,” amesema Swai.

Hakimu Huruma Shaidi amesema ni lazima amri za Mahakama zifuatwe. Ameahirisha kesi hadi Oktoba 13.

Amesema hadi siku hiyo, Sethi awe ameshapata matibabu na iwapo atakuwa hajapatiwa, mkuu wa gereza alipo afike mahakamani kujieleza.

Katika kesi hiyo, Sethi na James Rugemarila wanakabiliwa na mashtaka 12 ya uhujumu uchumi wakidaiwa kula njama, kujihusisha na mtandao wa uhalifu, kighushi, kutoa nyaraka za kughushi, kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu, kutakatisha fedha na kusababisha hasara ya Dola 22,198,544.60 za Marekani na Sh309,461,300,158.27.

Wanadaiwa kati ya Oktoba 18, 2011 na Machi 19, 2014 jijini Dar es Salaam walikula njama katika nchi za Afrika Kusini, Kenya na India ya kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.

CREDIT: MWANANCHI

KIONGOZI wa CUF Mheshimiwa Ali Juma Suleiman ambaye alikuwa Kaimu Mwenyekiti wa (CUF) Jimbo la Mto Pepo na Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa (CUF) Wilaya ya Magharibi A. Zanzibar amefariki dunia usiku wa kuamkia leo katika hospitali ya Mnazi Mmoja.

Baadhi ya viongozi wa (CUF) na wanachama pamoja na wananchi wakiwa katika hospitali ya Mnazi Mmoja kufuatilia mwili wa Marehemu Ali Juma Suleyman.

Naibu Katibu Mkuu (CUF) Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui amethibitisha kutokea kwa kifo hicho na kusema kuwa Mheshimiwa Ali Juma alikuwa amelazwa hospitali ya Mnazi Mmoja kufuatia kuvamiwa nyumbani kwake na kupigwa kisha baadaye kutupwa katika maeneo ya Masingini na makundi ya watu yanayoendesha vurugu Zanzibar.

"Nasikitika kutangaza kifo cha Mheshimiwa Ali Juma Suleiman, Kaimu Mwenyekiti wa CUF Jimbo la Mto Pepo na Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CUF Wilaya ya Magharibi A. Amefariki dunia majira ya saa 4 usiku hapa jana hapa Mnazi Mmoja Hospital baada ya kupigwa vibaya na Mazombi juzi usiku" alisema Naibu Katibu Mkuu CUF Nassor Mazrui

Viongozi wa CUF wamesema kuwa mwili wa marehemu umeshafanyiwa uchunguzi tayari na sasa wamekabidhiwa kwa ajili ya kufanya mazishi ambayo yatafanyika leo katika makaburi ya Mwanakwereke, nje kidogo ya mji wa Unguja. 

Unywaji wa pombe za kienyeji ambao wakati mwingine huambatana na baadhi ya wanywaji kufanya vurugu, ukatili wa kijinsia, uporaji na hata kujeruhi umemsukuma mkuu wa wilaya kuagiza itungwe sheria.

Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Chelestino Mofuga ameziagiza halmashauri mbili zilizopo wilayani humo zitunge sheria ndogo za udhibiti wa kutengeneza, kuuzaji na kunywa pombe hizo ili kukomesha matukio ya aina hiyo yanayotokea kila mara.

Mofuga alitoa agizo hilo juzi kwenye mkutano na wananchi uliolenga kukomesha matukio ya kikatili yanayosababishwa na unywaji wa pombe za kienyeji.

Alisema yapo matukio mengi ya kikatili yanayotokea sehemu tofauti katika eneo hilo yanayosababishwa na pombe za kienyeji, hivyo suluhisho ni utungwaji wa sheria ndogo.

Mkuu huyo wa wilaya alisema endapo halmashauri ya mji na ile ya wilaya zikitunga sheria ndogo, maeneo yaliyokithiri kwa pombe za kienyeji katika kata za Dongobesh na Sanu yatamalizika.

Alisema japo kuna sheria mama inayoongozwa na Katiba, kutungwa kwa sheria hizo kutapunguza matukio hayo.

Ofisa Maendeleo ya Jamii wa halmashauri ya wilaya hiyo, Melkiore Miniko alisema pia utungwaji wa sheria hizo utapunguza kwa kiasi kikubwa migogoro ya kifamilia.

Miniko alisema matukio ya kikatili yanasababisha na pombe haramu ya gongo na zingine za kienyeji zinazochangia kurudisha nyuma maendeleo.

Alisema wamekuwa wakipokea malalamiko mengi ya ukatili kwa watoto na kutelekezwa familia kunakotokana na wazazi wengi kujiingiza kwenye unywaji wa pombe haramu, hivyo suluhisho ni kuwapo na sheria ndogo. Ofisa huyo alisema kuwa licha ya kuwapo kwa sheria ya leseni ya vileo, inapaswa kuongezwa sheria ndogo ili kupunguza madhara hayo kwa jamii.

WATU wanaosadikiwa kuwa ni majambazi, wamevamia Msikiti Mkuu wa Ijumaa ulioko Kata ya Igunga Mjini wilayani hapa mkoani Tabora, kisha kumjeruhi mlinzi na kupora baadhi ya vitu ikiwemo vitabu vya dini ya Kiislamu.

Mlinzi aliyejeruhiwa ni Juma Mussa (55), mkazi wa Mtaa wa Nkokoto kata ya Igunga ambaye amelazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Igunga na hali yake bado ni mbaya. Mkuu wa Wilaya ya Igunga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya, John Mwaipopo alithibitisha kutokea kwa uhalifu huo na mtuhumiwa mmoja amekamatwa pamoja na vitu vilivyoibwa.

Alimtaja mtuhumia huyo kuwa ni Juma Mponi (45) ambaye ni mkazi wa Mtaa wa Stendi ya Mabasi mjini Igunga, na kutamba kuwa hakuna jambazi atakayetoka salama Igunga kwa kuwa polisi wamejipanga kikamilifu kukabiliana na matukio kama hayo.

Akizungumza kwa shida akiwa wodini, mlinzi huyo alisema shambulio hilo limetokea Septemba 25, mwaka huu saa 8 usiku, ambako watu hao walifika msikitini hapo kisha kurusha jiwe kwenye eneo alilokuwa amekaa.

Alisema baada ya kuona jiwe hilo, aliamua kusimama na mara jambazi mmoja aliruka uzio wa msikiti kisha akaingia na kuanza kumshambulia kwa mapanga kichwani. Alibainisha kuwa wakati akishambuliwa, aliona majambazi wengine wakifungua milango ya msikiti na mmoja wao akimweleza mwingine “wewe maliza kabisa huyo mlinzi.”

Hata hivyo, mlinzi huyo aliendelea kuuomba msaada kwa kupiga kelele ili asaidiwe, hali iliyowafanya majambazi kukimbia kusikojulikana wakiondoka na baadhi ya mali za msikiti. Mhasibu wa Msikiti Mkuu wa Ijumaa, Issa Said Feruzi alitaja vitu vilivyoibiwa na majambazi hao kuwa kuwa ni misahafu minne, feni moja, saa kubwa, vitabu vya hitima 30, kitabu cha mapato na matumizi, daftari za Tabligh nne, maikrofoni na stendi yake, miswala miwili; vyote vikiwa na thamani ya Sh 374,000.

Hata hivyo, alisema vitu vyote vimepatikana na viko Kituo cha Polisi Igunga; huku Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Igunga, Melchades Magongo amekiri kumpokea Juma Mussa, akieleza kuwa alimpokea hospitalini hapo akiwa na majeraha kichwani ambayo yanaonesha alikatwa na kitu chenye ncha kali. Dk Magongo alisema hali ya mlinzi huyo bado si nzuri akiendelea kupatiwa matibabu zaidi katika wodi namba nane hospitalini hapo.

Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema amemjia juu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi  na kusema Waziri huyo hana sifa za kuendelea kuwepo katika wizara hiyo kutokana na kuwa na majibu mepesi kuhusu matukio ambayo yanagharimu maisha ya watu.

Lema amesema hayo leo alipokuwa jijini Arusha akiongea na waandishi wa habari na kusema amesikitishwa sana na majibu ya Waziri Mwigulu Nchemba kuhusu sakata la miili ya watu kuokotwa baharini na sakata la shambulio la Tundu Lissu pamoja na kupotea kwa Ben Saanane ambaye alikuwa msaidizi wa Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe

"Mwigulu Nchemba amenisikitisha sana kwa kauli zake alizokuwa anatoa na sidhani kama anastahili kukalia ile ofisi hata kwa masaa 12 na ni wito wangu kwa Mhe. Rais Magufuli na naamini itakuwa hivyo hawezi kumuacha Waziri kama huyu kwenye ofisi ya serikali inayoshughulika na mambo ya ulinzi na usalama wa watu, matumaini yangu yupo hapo kwa muda tu, toka utamaduni wa maiti za watu kuanza kuokotwa zimeokotwa maiti za watu wengi sana lakini unaona kauli ya Waziri ni kama watoto wameokota maembe, amesema hawana mpango wa kuleta wachunguzi kutoka nje kuja kusaidia polisi kuchunguza tukio la Tundu Lissu hiyo ni hofu sababu wanajua nini kipo nyuma ya jambo hilo" alisema Lema

Aidha Mbunge huyo amesema kuwa kitendo cha Waziri Mwigulu Nchemba kusema gari ambayo alikuwa anailalamikia Mbunge Tundu Lissu na yeye kusema gari hiyo imeonekana Arusha na haijawahi kutoka Arusha bila kuchukuliwa hatua yoyote ni jambo ambalo linaibua maswali mengine na kufanya wazidi kukosa imani na jeshi la polisi kuhusu kuchunguza sakata la Tundu Lissu.

"Gari ikiwa inatuhumiwa Waziri hasemi kuwa gari hiyo imeonekana Arusha na haijawahi kutoka Arusha ila gari ikiwa inatuhumiwa cha kwanza watu wanatakiwa kuwajibika lakini ukweli ni kwamba watu wanatumia namba feki kwa ajili ya matukio, jana Waziri anaongea vitu vyepesi mimi nasema siku za Waziri huyu kukaa pale kama Waziri wa Mambo ya Ndani siku zake zinahesabika na nyinyi mtaniambia, anasema hajui kama Ben Sanane amekufa au hajafa kama mpaka leo Waziri wa Mambo ya Ndani hajui juu ya Ben Sanane kama amekufa au yuko hai polisi hawa tunasema hawawezi kuchunguza sakata la shambulio la Tundu Lissu ndiyo maana tunataka uchunguzi kutoka nje ya nchi waje kusaidia jambo hili" alisema Godbless Lema

NA CHRISTINA MWAGALA, OFISI YA MEYA WA JIJI

MSTAHIKI Meya wa jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita amekutana na ugeni kutoka Jiji la Shanghai nchini China na kujadili mambo mbalimbali yamaendeleo jijini hapa ikiwemo suala la uboreshaji wa kituo cha Mabasi Ubungo.

Ugeni huo uliambatana na Meneja Mkuu wa Kampuni ya Linghang Cathy Wang ambayo ndiyo imeingia mkataba na Halmashauri ya jiji kwa ujenzi wa kituo hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa mara baada ya kumalizika kwa mazungumzo hayo, Meya Mwita alisema kuwa ugeni huo umeridhia kuwekeza katika nyanja mbalimbali ikiwemo kituo cha mabasi ubungo.

Alifafanua kuwa jiji la Dar es Salaam linakaribia kunza kwa ujenzi wa mradi mkubwa wa kubadilisha kituo cha mabasi ubungo na kwamba hatua mbalimbli zimeshakamilika ili kupisha mradai huo.

Alisema kuwa mara baada ya kukamilika kwa mradi huo jumla ya watanzania 20,000 watapata ajira jambo ambalo litawezesha kuongeza kipato kwa wananchi na hivyo pia kuwezesha vijana kuondokana kwenye makundi ambayo sio salama.

Alisema kufanikisha kwa mradi huo, utasaidia pia kuongeza mzunguko wa fedha jijini hapa kutokana na kuwepo kwa fursa nyingi za kibiashara.

“ Leo nimekutana na ugeni ambapo kwa kiasi kikubwa mnafahamu ndugu zetu hawa wamekuwa na urafiki mkubwa katika nchini yetu, tumejadiliana mambo mengi ambayo yote ni yakuleta maendeleo katika jiji letu.

“ Lakini kubwa zaidi ni kuhusu ujenzi wa kituo cha mabasi Ubungo, ambapo hivi karibuni tunatarajia kuanza kwa mradi huo, na wananchi pia watajulisha, nitumie fursa hii kuwaeleza wananchi kuwa jiji linafuata utaratibu katika kutekeleza mradi huo” alisema Meya Mwita.

“ Fursa hii ni kubwa ambayo tumeipata, watanzania watapata ajira, mzunguko wa fedha kwenye jiji letu utaongezeka, kama Meya wa jiji hili nimewakaribisha tufanye kazi pamoja, lengo likiwa nikuweka jiji kwenye muonekano mzuri” aliongeza.

Kwaupande wake Meneja Mkuu wa Kampuni ya Linghang Cathy Wang alimpongeza Meya Mwita kutokana na aina ya utendaji wake wa kazi nakuahidi kuonyesha ushirikiano katika utekelezaji wa mradi huo.

Alisema kuwa Meya Mwita ni kiongozi anayefanya kazi kwa bidii na umakini na kwamba kutokana na jitihada hizo za kulijenga jiji , kampuni yao itafanya  kazi na kumuhakikisha kufanya kazi kwa ushirikiano mkubwa






MGAN
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mh. Hamisi Kigwangalla amemwagiza mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya Butiama mkoani Mara, Saimon Ngiliule kumsimamisha  kazi mara moja Tabibu Danieli Mtatiro wa kituo cha Afya  Kiagata kwa tuhuma za kula pesa za wanakijiji kiasi cha sh.2 milioni zilizotokana na malipo ya mfuko wa Afya ya Jamii (CHF).                
   Pia Dk. Kigwangalla amemwagiza Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na rushwa (TAKUKURU) kumkamata tabibu huyo ili kuhojiwa na kuchukuliwa hatua. “Nakuagiza Mkurugenzi msimamishe kazi Bwana Mtatiro na afikishwe TAKUKURU haraka sana. Huku ni kuujumu mpango wa serikali wa kuwaletea maendeleo kupitia afya matokeo yake mtu mmoja anachukua pesa za wananchi wanaozipatia taabu hali inayowafanya wakose matibabu” amesema Dk. Kigwangalla.              
Dk. Kigwangalla ambaye yupo katika ziara ya kuimalisha sekta ya Afya Wilaya za Butiama na  Serengeti mkoa wa Mara  pia ameweza kukagua hospitali ya wilaya Butiama pamoja na kuzuru kaburi la Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.
Dk. Kigwangalla yupo katika ziara yake ya kikazi ya siku mbili Wilayani Butiama na Serengeti. ambapo anakagua vituo vya Afya, Zahanati na Hospitali ikiwa katika mpango wa uboresha wa Sekta ya Afya

ummy-mwalimu2Ugonjwa wa Kichaa cha Mbwa ni mojawapo ya magonjwa yaliyoathiri nchi yetu na maeneo mengi duniani.  Ugonjwa huu husababishwa na virusi kutoka kwa wanyama jamii ya mbwa ambao wameathirika na virusi hivi (Mbwa, paka, mbweha, fisi na wengineo) na humwingia mwanadamu kwa kuumuuma na mate ya mnyama yenye virusi hivi huingia  katika eneo lenye jeraha.
Takwimu za kidunia zinaonyesha ugonjwa wa Kichaa cha Mbwa inakadiriwa kusababisha takribani vifo 59,000 ambapo kati ya hao, asilimia 36 hutokea katika bara la Afrika.  Inakadiriwa kuwa kati ya 30%-50% ya waathirika wa kichaa cha mbwa ni watoto chini ya miaka kumi na tano. Pamoja na kusabisha vifo, ugonjwa huu pia unasababisha athari kubwa katika kiuchumi kwani chanjo ambayo ndio matibabu yake ni kubwa.  Gharama ya chanjo inakadiriwa kuwa 150,000 kwa mgonjwa kwa bara la AfriKa, ambayo ni sawa na 6% ya mapato ya nchi katika bara hilo.
Kwa hapa Tanzania, ugonjwa wa kichaa cha mbwa uliripotiwa kwa maara ya kwanza mnamo 1932/33. Baada ya hapo, wagonjwa wameendelea kuripotiwa kutoka maeneo mbalimbali ya nchi kwa viwango tofauti. Kwa mwaka huu kati ya mwezi Januari hadi Agosti, watu 17,326 wametolewa taarifa ya kuumwa na mbwa au wanyama wa jamii  hiyo na kumetokea vifo 8.  Takwimu hizi hazijumuishi vifo vinavyotokea nyumbani na waathirika ambao hawakufika katika vituo vya kutolea huduma za afya, hivyo tatizo hili ni linaweza pia kubwa kuliko tunavyofikiri. Utafiti uliofanyika mwaka 2002 ulibainisha kuwepo na uwezekano wa kuwepo takriban vifo 1,499 kwa mwaka nchini kutokana na ugonjwa huu.
Tafiti pia zimeonesha waathirika wakuu wa ugonjwa huu ni watoto chini ya miaka 15. Uwezekano mkubwa ni kwa sababu wao ndio wanaokuwa karibu na mbwa(anaefugwa) muda mwingi, na pia hupenda kucheza/kuchokoza mbwa wasiowafahamu njiani.
Vimelea vya kichaa cha mbwa vinapoingia katika jeraha hushambulia neva za fahamu kutoka katika eneo la jeraha, kuelekea katika uti wa mgongo na hatimae kuathiri ubongo. Dalili huanza kuonekana baada ya kuathirika kwa mfumo wa kati wa fahamu, na baadae ubongo, ambazo ni pamoja na kuwashwa sehemu ya jeraha, homa, kuumwa kichwa, maumivu ya mwili,  kuogopa maji na mwanga, kutokwa mate mengi mfululizo, kuweweseka (kushtuka mara kwa mara na kuogopa), kupooza na hatimae kupoteza maisha. Wakati mwingine watu huhusisha dalili hizi na imani potofu.
Katika juhudi za kudhibiti ugonjwa huu, Tanzania ilipata ufadhili wa Bill na Melinda Gates na kushirikiana na Shirika la Afya Duniani na kuwa moja ya nchi zilizochaguliwa kutekeleza  ‘Mradi wa majaribio wa Kutokomeza Kichaa cha Mbwa’ kati ya mwaka 2009-2016, nchi nyingine zikiwa ni Ufilipino na Afrika ya Kusini. Lengo kubwa la mradi huu lilikuwa ni kusaidiana na nchi hizi katika kutokomeza ugonjwa huu kwa jamii ya mbwa na paka ili wawe na virusi hivi  endapo watamuuma binadamu. Utekelezaji wa mradi ulihusisha kampeni za kuchanja mbwa wote kwa mwaka mara moja. Aidha, chanjo za binadamu pia zilitolewa. Mradi huu ulitekelezwa katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro Lindi na Mtwara, ambapo mbwa na paka walipatiwa chanjo kila mwaka. Katika mradi huu:
  • Chanjo za binadamu dozi 28,000 zilitolewa katika eneo la mradi.
  • Watumishi 101 walipata mafunzo kuhusu rabies na njia mpya ya utoaji chanjo, na jinsi ya kuhakikisha hakuna ‘kuishiwa na chanjo’.
  • Mwongozo wa Kudhibiti Kichaa cha Mbwa kwa wanafunzi wa shule za msingi uliandaliwa.
  • Elimu ya afya kuhusu kichaa cha mbwa na jinsi ya kujikinga ilitolewa kwa jamii kupitia kampeni za uchanjaji.

  • Vielimishi jamii vilitengenezwa na kusambazwa. Kufuatia mradi huu, vifo vinavyotokana na Kichaa cha mbwa katika maeneo ya mradi vilipungua toka 17 mwaka 2010 hadi 0 mwaka 2013 hadi 2015.
Kama ilivyoelezwa hapo juu, ugonjwa huu hutoka kwa wanyama jamii ya mbwa/paka aliyeathirika na virusi hivi na kuja kwa binadamu anapomuuma. Hivyo juhudi za pamoja zinahitajika kwa sekta zote mbili ili kutokomeza ugonjwa huu.
Mambo muhimu ya kufanya ili kujikinga:
  1. Endapo mtu ameumwa na mbwa, hatua ya kwanza muhimu ni kuosha jeraha kwa dakika 10 au zaidi kwa maji mengi yanayotiririkika na sabuni.

  2.  Kidonda kisifungwe. Kisha apelekwe haraka katika ktuo cha kutolea huduma za afya ili kupata chanjo ya kichaa cha mbwa. 
  3. Ni muhimu aliyeumwa na mbwa afanyiwe tathmini ya kina katika kituo cha kutolea huduma ili aweze kupatiwa chanjo kamili na iwapo chanjo ikitolewa ni budi kumaliza kozi zote za chanjo.

  4.  Wizara imekwisha kutoa maagizo kwa mikoa na wilaya kuhakikisha kuwa chanjo hizi zinanunuliwa  na kutolewa kwa wananchi wanaozihitaji.

  5. Mtu aliyeumwa na kichaa cha mbwa awahi kituo cha kutolea huduma za afya na kupata chanjo dhidi ya ugonjwa huo, na ni muhimu kumaliza kozi.

  6. Wanyama jamii ya mbwa, paka wasiruhusiwe kulamba vidonda, kwani mate yao huweza kuleta maambukizi endapo wameathirika.

  7. Wamiliki wa mbwa wahakikishe wanachanja mbwa wao dhidi ya kichaa cha mbwa mara moja kila mwaka na kupata cheti.

  8. Mbwa wafungiwe ndani wakati wa mchana na wasiachwe kuzurura hovyo, kwani wanaweza kupata maambukizi endapo watakutana na mnyama aliyeambukizwa.

  9. Kuhakikisha mazingira yote ni safi, ili kutowapa chakula mbwa wanaozurura mtaani na kuzoea kuja katika mazingira tunamoishi.
  10. Watoto wapewe elimu na wakatazwe kuchokoza mbwa  wasiowajua njiani (kuvuta mkia/masikio, kumpanda mgongoni n.k)
Katika kutekeleza mikakati na juhudi za pamoja za sekta zote zinazohusika kudhibiti ugonjwa huu, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto imeshirikiana na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Shirika la Afya Duniani, Shirika linaloshughulika na Afya ya Wanyama Duniani (OIE) na asasi zisizo za kiserikali katika kuandaa ‘Mkakati wa Kudhibiti Kichaa cha Mbwa’ wenye lengo la kutokomeza ugonjwa huu ifikapo 2030. 
Tunawapongeza wote wanaoshiriki kwa njia moja au nyingine katika kudhibiti kichaa cha mbwa, na tunazidi kutoa wito kwa jamii kwa ujumla kuzingatia maelekezo ya kuzuia/kujikinga na ugonjwa huu. Tunatoa shukrani kwa wadau mbalimbali wanaoshiriki nasi katika juhudi hizi- Mfuko wa Bill na Melinda Gates,  Shirika la Afya Duniani, Shirika la Wanyama, Taasisi ya Afya Ifakara na wengineo.

MKRdezign

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget