Kitaifa, Kimataifa, Siasa, Michezo na Burudani

Makamu wa Rais Mgeni Rasmi Kongamano la Kimataifa la Jinsia


samia-hassan-suluhu
Na Husna Saidi-MAELEZO
Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Kimataifa la Jinsia na Usawa Katika Jamii  lililoandaliwa na Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) Aprili 27 mpaka 28 mwaka huu  chuoni hapo.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na  Afisa Habari, Elimu na Mawasiliano wa Chuo hicho Lila Mandu  alipokuwa akiongea na waandishi wa habari kuhusu lengo la kongamano hilo.
Mandu alisema lengo kuu la kongamano hilo ni kuchunguza kwa kina masuala mbalimbali ya kijinsia pamoja na kubaini mbinu bora za kuondoa ukosefu wa usawa wa jinsia katika muktadha wa Taasisi za Elimu ya Juu.

“Tutatathmini sababu na changamoto zinazosababisha ukosefu wa usawa wa kijinsia katika Taasisi za Elimu ya Juu kwa kutumia mifano mizuri kutoka Taasisi zingine ambazo zinajitahidi kuhamasisha usawa na haki za wanawake na wanaume pia,” alisema Mandu.
Aliendelea kwa kusema kuwa kongamano hilo litabainisha fursa za kimkakati katika kuwahusisha wadau wa masuala ya jinsia katika kuhamasisha usawa na haki za watu wote ambapo  litakuwa na washiriki 140.
Aliwataja washiriki hao kuwa ni wasomi kutoka DUCE, Taasisi na vyuo mbalimbali ndani na nje ya nchi, wanafunzi wa shahada za uzamili na uzamivu katika masuala ya jinsia, wawakilishi wa mashirika ya haki za binadamu, watunga sera pamoja na wasomi wanaotambulika Kimataifa katika masuala ya jinsia.
Kwa upande wake, Mratibu Kitengo cha Jinsia DUCE Fatma Hamad alisema licha ya maovu wanayotendewa wanawake kuendelea kujitokeza hapa nchini, kongamano hilo litasaidia kutoa elimu ya jinsia na usawa ili kusaidia Serikali na wananchi kwa ujumla kuondokana na hadha hiyo.
Chuo cha DUCE pamoja na waandaaji wa kongamano hilo wamealika wadau mbalimbali wa masuala ya jinsia, wasomi, waandishi wa habari na wananchi kwa ujumla kushiriki katika kongamano hilo.
Labels:

Post a Comment

[facebook]

MKRdezign

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget