Kitaifa, Kimataifa, Siasa, Michezo na Burudani

WANASHERIA WATAKA MFUMO WA SHERIA ZA KIMATAIFA ZA MADINI UCHUNGUZWE


kilangi
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.

Mtaalam mbobevu wa Sheria za Madini na Mafuta nchini, Dkt. Adelardus kilangi ametoa rai kwa wanasheria watakaoteuliwa kwa ajili ya kurekebisha Sheria za Madini kuanza kufanya kwanza uchunguzi katika  Sheria za Kimataifa za Madini ili waweze kuishauri vizuri serikali.

Rai hiyo imetolewa leo na mtaalam huyo katika mahojiano maalum na mwandishi wa habari hii kuhusu maoni juu ya ripoti ya uchunguzi wa mchanga wa madini iliyowasilishwa na baadhi ya wachumi pamoja na wanasheria walioteuliwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

Dkt. Kilangi amesema kuwa ripoti iliyowasilishwa imeonesha madhaifu yaliyopo katika sekta ya madini ambayo madhaifu hayo yamegawanyika katika maeneo ya mfumo wa Sheria pamoja na mfumo wa usimamizi ambapo tatizo kubwa limekuwa ni kukosa uzalendo kwa viongozi waliopewa dhamana ya kufanya maamuzi ya nchi.

“Katika eneo la mfumo wa Sheria, kwanza nampongeza Rais Magufuli kwa kuwataka wanasheria na wataalamu wengine kufanya mapitio ya Sheria hizo kwa sababu tukitaka kuleta mabadiliko lazima tuanzie kwenye Sheria hivyo kwa kutengeneza Sheria nzuri zenye manufaa kwa umma ni lazima tuanzie katika ngazi za kimataifa kwani kuna vipengele vinavyoathiri sekta yetu ya madini,”alisema Dkt. Kilangi.

Mtaalamu huyo ameongeza kuwa ni lazima kufahamu kwanza mfumo wa Sheria za kimataifa kwa sababu  nchi zilizoendelea zimetengeneza kwa makusudi Sheria kandamizi kwa nchi  zinazoendelea.

Amefafanua kuwa, kabla ya kuanza kuchunguza Sheria zetu za ndani wanasheria lazima wafahamu jinsi mifumo hiyo mitatu inavyofanya kazi na inavyoathiri sekta yetu ya madini, yaani sheria za kimataifa ikiwemo ya Sheria za Kimapokeo/kimila za kimataifa (Customary International Law), Mikataba inayoingiwa na mataifa mbalimbali (Multilateral Framework) pamoja na mikataba inayosainiwa kati ya nchi mbili (Bilateral Framework).Baada ya hapo ndio waje kwenye sheria zetu za ndani na hatimaye mikataba kati ya serikali na wawekezaji.

Katika mapendekezo mengine, Dkt. Kilangi alisema kuwa wasomi wanasheria na wataalamu wengine kama wachumi wanatakiwa wapambane kisomi, wapewe hoja za kupambana na mfumo gandamizi uliopo katika Sheria za kimataifa uliotengenezwa na mataifa makubwa, na kutafuta mbinu za kupanga upya Sheria za madini nchini kwa kuongozwa na mapungufu yaliyojitokeza katika ripoti mbili za mchanga wa madini, tafiti mbalimbali pamoja na mitazamo kutoka nchi zingine juu ya mambo wanayoyaangalia katika kubadilisha sheria zinazofanana na hizo.

Aidha, amependekeza wanasheria kufanya  marejeo haya kwa kuangalia pia falsafa ya uchumi inayopaswa kutuongoza kwa kuangalia ufahamu wetu kama taifa kuhusu njia kuu za uchumi na  nyenzo kuu za uzalishaji (Political Economy Analysis) ambapo wataweza kufahamu nani anamiliki njia kuu za uchumi, nani anamiliki rasilimali, nani anatoa mtaji, nani anafanya kazi, nani anazalisha na  , faida inapatikana kiasi gani, na nani anaipata faida hiyo, hali itakayopelekea muwekezaji kuingia ubia mzuri na Serikali. Haya yote yafanywe kwenye muktadha wa sekta ya madini.

Pia Dkt. Kilangi alisisitiza kuwa katika mchakato huo wa kurekebisha sheria za madini ni vizuri kushirikisha wananchi wa kawaida ili kupata maoni yao, kwani nao tayari wameshafahamu athari za mikataba iliyopo sasa, na kwa kweli haya madini ni yao. Kwa hiyo kuhusishwa kwao ni muhimu alisisitiza.

Labels:

Post a Comment

[facebook]

MKRdezign

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget