Kitaifa, Kimataifa, Siasa, Michezo na Burudani

RC TABORA MAAFISA UGANI KUWENI MASHAMBA DARASA AMBAYO WAKULIMA WAKUJA KUJIFUNZA KUTOKA KWENU ULIMAJI BORA WA TUMBAKU


Na Tiganya Vincent, RS-TABORA

Maafisa Ugani wa Kata, Vijiji na Wilaya zote zinazolima tumbaku mkoani Tabora wametakiwa kuwa na mashamba darasa ambayo wakulima watayatumia kama sehemu ya kwenda kujifunza juu ya uzalishaji wa tumbaku kwa tija na  ubora unaotakiwa ili waweze kuongeza kipato chao.

Kauli hiyo ilitolewa jana katika Chuo cha Mafunzo ya Kilimo Tumbi na Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri wakati akifungua mafunzo ya siku sita ya  Maafisa Ugani 114  yakiwa na lengo la  kuwajengea uwezo wa kusimamia vizuri zao la tumbaku na wakulima wake.

Alisema kuwa baada ya mafunzo hayo ni jukumu la Wataalamu kwenda kuwasaidia wakulima  wa tumbaku ili wabadilike katika kilimo chao kwa ajili ya kuondokana na unyonge wa uzalishaji ambao haumpi mazao na bei nzuri katika masoko ya tumbaku.

Bw. Mwanri alisema kuwa zoezi hilo ni pamoja na Maafisa hao kuwa karibu na wakulima kuanzia wakati wa matayarisho ya vitalu hadi wanapokuwa wanapokwenda tumbaku yao katika masoko ili kama kuna matatizo yanayowakwamisha waweze kuwasaidia.

Alisema kuwa sanjari kuwa karibu na wakulima Maafisa hao ni lazima kuanzia msimu ujao wa kilimo wapite kwa kila mkulima ili kuhakiki mazao yaliyopo katika mashamba ya wakulima wa tumbaku  (crop survey) ili kujua hali halisi ya matarajio ya uzalishaji wa kila mmoja wao kwa ajili kuepuka udanganyifu.

Bw. Mwanri alisema kuwa hatua hiyo itasaidia kuwabaini watu ambao hawakulima tumbaku lakini inapofika msimu wa mauzo wanaingiza tumbaku katika masoko na kuendelea kuwanyonya wakulima na kuwafanya waendelee kuwa tegemezi.

Naye Mkuu wa Chuo cha Kilimo Tumbi Kasele Steven alisema kuwa Mafunzo hayo ya siku kwa Maafisa Ugani hao ni muhimu sana katika kuhakikisha kuwa wanapata elimu itakayowawezesha kuwa na uelewa wa kutosha juu ya zao hilo kwa sababu baadhi yao wakati wanasoma vyuo hawakupata mafunzo kuhusu zao la tumbaku.

Alisema kuwa baada ya mafunzo hayo Maafisa Ugani wa Serikali watakuwa karibu sana na wakulima kuliko ilivyokuwa hapo awali ambapo ni Maafisa Ugani wa Kampuni za Tumbaku pekee ndio walikuwa wakimhudumia mkulima wa tumbaku na kukosa msaada wa Wataalamu wa Serikali.

Steven aliongeza kuwa Maafisa Ugani wataweza kujifunza juu ya aina na sifa za mbegu bora za tumbaku, uandaaji na utunzaji wa vitalu , maandalizi ya shamba, utunzaji wa shamba, uvunaji wa tumbaku, ukaushaji wa tumbaku ,uchambuzi na upangaji madaraja ya tumbaku na Sheria na Kanuni za kilimo cha tumbaku.

Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa magizo la Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa aliyoyatoa alipofanya ziara mkoani hapo kwa vipindi tofauti tofauti ya kutaka Maafisa hao wapatiwe mafunzo na waende kuwasaidia wakulima wa tumbaku badala ya kuwaachia wa Kampuni zinazonunua Tumbaku pekee ndio wahudumie mkulima wa tumbaku.

Katika kutekeleza agizo hilo Mkoa wa Tabora umeanza na Maafisa Ugani 114 ambao wanatoka Wilaya za Sikonge, Nzega, Uyui, Manispaa ya Tabora, Urambo , Kaliua na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora.

Labels:

Post a Comment

[facebook]

MKRdezign

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget