Jovina Bujulu,MAELEZO.
Hivi
karibuni , Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wazee na
Watoto, Mh. Ummy Mwalimu ameagiza Halmashauri zote nchini kuwaadalia na
kuwapa wazee vitambulisho vya kupata huduma za matibabu bila malipo
katika hospitali , vituo vya afya na zahanati za umma katika maeneo
yao.
Waziri
Ummy amewapa muda hadi kufikia Desemba 30, mwaka huu wawe wametekeleza
agizo hilo. Kwa kuzingatia na usumbufu ambao wazee wamekuwa wakiupata
wanapokwenda kupata matibabu katika vituo vya afya utekelezaji wa agizo
hilo litakuwa ni mkombozi kwao ili nao wapatiwe matibabu yanayostahili.
“Baadhi
ya wazee wamekuwa wakipata tabu ya kupata huduma bora katika hospitali
za umma, natoa wito kwa wakurugenzi kupunguza kadhia wanayopata wazee
hao wanapokwenda kutibiwa , hakikisheni mnawapatia vitambulisho wazee
wote wasiokuwa na uwezo “ alisema Waziri Ummy.
Vitambulisho
hivyo vitawapa fursa ya kutibiwa bure na hivyo watapata motisha ya
kwenda kupata matibabu katika hospitali mbalimbali bila kutoa malipo
yoyote. Kabla ya agizo hilo wazee kuanzia miaka 60 walikuwa wanalazimika
kupata barua kutoka kwa watendaji wa Serikali za Mtaa ili waweze
kutibiwa bure
Utaratibu
huu kwa kiasi kikubwa ulikuwa na usumbufu ambapo walikuwa wanatakiwa
kwenda kuchukua barua kwa Watendaji wa Serikali za Mitaa kila
wanapoumwa na barua hizo zilikuwa zinawawezesha kutibiwa bure kwa
wakati huo na endapo wataumwa tena wanalazimika kufuata barua tena.
Serikali
ilifanya uamuzi wa kuwa na Sera ya Wazee mwaka 1999, katika maadhimisho
ya mwaka wa Kimataifa wa Wazee. Maamuzi hayo yalikuwa ni kielelezo cha
dhamira ya Serikali ya kuweka masuala ya wazee katika agenda za
maendeleo ya nchi yetu.
Pamoja
na kuwa Serikali inawatambua wazee kuwa ni rasilimali na hazina kubwa
katika maendeleo ya nchi yetu, wazee hao wanakabiliwa na matatizo ya
umaskini, kutotosheleza kwa huduma za afya, pensheni na kutoshirikishwa
katika maamuzi yanayohusu maendeleo ya nchi yetu. Wazee wengi huishi
katika hali ya umaskini inayoleta mashaka makubwa kwao na takribani
asilimia 75 wazee wanaishi vijijini.
Taarifa
za Umoja wa Mataifa za mwaka 1999, zinaonyesha kuwa katika Afrika ,
Tanzania ni nchi ya pili kuwa na sera ya wazee baada ya nchi ya
Mauritius.
Kupitia
Sera hiyo Serikali iliahidi kuhakikisha kuwa wazee wanatambuliwa na
wanapata fursa ya kushiriki katika maendeleo ya nchi sambamba na
wananchi wengine.
Aidha
taarifa hizo zinaendelea kuonyesha kuwa kumekuwa na ongezeko la idadi
ya wazee duniani na hasa katika nchi zinazoendelea ambapo viwango vya
ongezeko havilingani na uwezo wa rasilimali zilizopo kuwahudumia katika
nyanja za afya, lishe, na huduma nyingine za msingi kwa maisha ya
binadamu.
Takwimu
zinaonyesha kuwa mwaka 1950, Umoja wa Mataifa ulikadiria kuwepo kwa
watu milioni 200 wenye umri zaidi ya miaka 60, na mwaka 1975, idadi
iliongezeka kufikia milioni 350 na ilitegemea kuongezeka kufikia milioni
625, ifikapo mwaka 2005 na idadi hiyo itazidi idadi ya vijana na watoto
wenye umri wa miaka 24 ifikapo mwaka 2050.
Barani
Afrika idadi inategemea kuongezeka kutoka milioni 38 za mwaka 1999, na
kufikia milioni 212 ifikapo mwaka 2050. Kwa kuangalia ongezeko hilo la
wazee ni wakati muafaka wa kuwapatia vitambulisho ili kuwapunguzia adha
ya kupata huduma za afya.
Sera
ya Taifa ya Afya na Sheria ya Utumishi wa Umma nchini Tanzania
zinazingatia umri wa miaka 60 kuwa ndio kigezo cha uzee , hivyo kwa
sera hii mzee ni mtu mwenye wa miaka 60 na kuendelea. Madhumuni ya sera
hii ni pamoja na kuwatambua kama rasilimali muhimu katika maendeleo ya
Taifa letu na kuhakikisha kuwa wazee wanapata huduma zote za msingi
zikiwemo huduma za afya.
Nchini
Tanzania wazee wapo katika makundi mbalimbali ambayo ni wazee wastaafu,
wakulima, wafugaji wavuvi na wale wasio na ajira ambao kuzeeka kwao ni
matokeo ya kupungukiwa nguvu za kufanya kazi.
Mazingira
ya wazee hao ni pamoja na matunzo duni, umaskini, magonjwa ya muda
mrefu, lishe duni , huduma za afya kuwa ghali na wao kushindwa kuzimudu,
na kuhitaji uangalizi na matunzo maalum ya kitaalamu.
Kwa
kuanzisha utaratibu wa kutoa vitambulisho vya matibabu kwa wazee ,
Serkali imetekeleza ahadi ya kurekebisha Sera ya kuchangia gharama za
afya kwa kurekebisha vigezo vya utambuzi wa umri wa miaka 60 na kuweka
utaratibu wa kufuatilia afya za wazee katika jamii.
Wazee
wote wenye sifa za kuwa na vitambulisho hivyo ni budi wajitokeze kwa
wingi ili waweze kupatiwa na kuwaondolea kabisa adha ya kupata huduma
za matibabu katika hospitali za umma.
Post a Comment