Kitaifa, Kimataifa, Siasa, Michezo na Burudani

Viongozi Jumuiya ya Afrika Mashariki Watakiwa Kutanguliza Mbele Maslahi ya Taifa.


Na Beatrice Lyimo
Aliyekuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli ametoa wito kwa nchi zinazokinzana ambazo zipo ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kutanguliza maslahi ya Taifa mbele na kuweka nyuma maslahi binafsi kwa maendeleo ya nchi.
Wito huo ameutoa jana jijini Dar es Salaam wakati wa Mkutano wa 18 wa Wakuu wa nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, alipokuwa akibainisha baadhi ya mafanikio yaliyopatikana ndani ya uongozi wake.

Rais Magufuli ambaye amemaliza muda wake wa Uenyekiti wa Jumuiya hiyo alisema kuwa, katika uongozi wake  Jumuiya imejitahidi kupunguza uhasama miongoni mwa pande zinazokinzana hususani katika  nchi za Burundi na Sudani ya Kusini.
“Nitoe pongezi za dhati kwa msuluhishi wa mgogoro wa Burundi, Rais Museven pamoja na mpatanishi wa mgogoro huo Rais Mstaafu wa Tanzania Benjamin Mkapa wamefanya kazi kubwa sana,” alisema Dkt. Magufuli.
Aidha, alibainisha baadhi ya mafanikio yaliyopatikana katika uongozi wake ambapo kumekuwa na maendeleo ya miundombinu ikiwemo usafiri ambapo kumekuwa na miradi mbalimbali ya barabara iliyokamilika na mengine tayari imeshafanyiwa upembuzi yakinifu.
Vilevile, Rais Magufuli amesema kuwa kumekuwa na mafanikio katika utekelezaji wa agenda ya utangamano ambapo utekelezaji wa eneo la ushuru wa forodha unaendelea vizuri.
“Katika kipindi chetu cha uongozi tumeweza kusimamia utekelezaji wa  baadhi ya masuala yanayohusu soko la pamoja ambapo limeanza kutekelezwa,kuhusu ushirikiano wa  fedha tumeweza kufanikisha uandaaji wa miswada miwili ambayo ipo tayari kupelekwa katika Bunge la Afrika Mashariki,” alifafanua Rais Magufuli.
Akifafanua zaidi Rais Magufuli amesema kuwa katika suala la utawala bora na demokrasia Jumuiya imepiga hatua katika eneo hili ambapo utawala bora na mambo ya kidemokrasia yameimarika, pia kukuza uhusiano baina ya Jumuiya na wadau wa maendeleo..
Mbali na hayo Dkt. Magufuli alibainisha baadhi ya changamoto zilizojitokeza katika uongozi wake ikiwemo suala la Mkataba wa Ushirikiano wa Kiuchumi(EPA) ambapo Jumuiya haikuweza kusaini mkataba huo.
Kwa upande wake Rais wa Uganda Yoweri Kaguta Museven ambaye kwa sasa ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ameshukuru kwa kuaminika na kuweza kuchaguliwa kuongoza Jumuiya hiyo.
Aidha, Rais  Museven amebainisha baadhi ya masuala ya kuzingatia ili kuweza kuimarisha uhusiano uliopo baina ya nchi hizi za Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwemo  Ustawi wa Maendeleo, Undugu na Ulinzi .
“tunapoongelea kuhusu Jumuiya ya Afrika Mashariki, tunaongelea juu ya ustawi wa maendeleo yetu, familia yetu, nchi zetu na hata soko letu, hivyo yatupasa kuzidisha utangamano kwa maendeleo ya Jumuiya,” amesema Rais Museven.
Wakati huo huo katika Mkutano huo baadhi ya viongozi wa Jumuiya hiyo waliapishwa. Viongozi hao ni pamoja na Rais wa Mahakama kuu ya Afrika Mashariki Jaji Charles Oyo Nyawelo na Naibu Katibu Mkuu Mhandisi Steven Malekela Mlote aliyechukua nafasi ya Enos Bukuku aliyemaliza muda wake.
Mbali na hayo katika Mkutano huo washindi wa shindano la kuandika insha kwa wanafunzi wa shule za Sekondari za EAC walikabidhiwa zawadi zao ikwemo vyeti na fedha kama motisha ambapo mshindi wa kwanza anatoka nchini Burundi alikabidhiwa fedha za Dolla za Kimarekani 1500.
Labels:

Post a Comment

[facebook]

MKRdezign

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget