Kitaifa, Kimataifa, Siasa, Michezo na Burudani

Prof. Mbarawa kuhusu wanaodai fidia kwa serikali kupisha ujenzi wa barabara



Serikali imesema itawalipa fidia kwa mujibu wa sheria wananchi wote waliopisha ujenzi wa barabara katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Amesema hayo Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa wakati akizungumza na wananchi wa Mwigumbi mkoani Shinyanga alipokagua ujenzi wa barabara ya Mwigumbi – Maswa yenye urefu wa KM 50.3 inayojengwa kwa kiwango cha lami na mkandarasi wa Kampuni ya CHICO na kuridhishwa na kasi ya ujenzi wake ambao unagharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 61.
“Kila anayestahili kulipwa fidia atalipwa kama sheria inavyoelekeza na endapo akatokea yeyote mwenye malalamiko Serikali ipo itamsikiliza,” amesema Waziri Prof. Mbarawa.
Amewataka wananchi kutoa ushirikiano kwa Mkandarasi na Viongozi wa Wakala wa Barabara (TANROADS), wa mkoa ili kuhakikisha barabara hiyo inakamilika kwa wakati na spidi inayotakiwa.
Aidha, Waziri Prof. Mbarawa amewahimiza makandarasi wote nchini kutoa kipaumbele cha ajira kwa wakazi wa maeneo husika inapopita miradi ya maendeleo ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali ili kuwapatia kipato na kuinua uchumi wao.
Naye, Kaimu Meneja wa TANROADS mkoa wa Shinyanga Eng. Batholomeo Ndirimbi, amesema mpaka sasa tayari fedha zimetengwa kwa ajili ya ulipaji fidia na watahakikisha kuwa fedha hizo zinalipwa kwa watu sahihi wanaostahili fidia hizo.
“Tutasimamia zoezi hili kwa umakini na kutoa fidia kwa wale wote wanaostahili kisheria,” amesema Eng. Ndirimbi.
Ameongeza kuwa ujenzi wa barabara hiyo umefikiwa asilimia 77 na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka huu.
Katika hatua nyingine, Waziri Prof. Mbarawa amekagua mradi wa ujenzi wa barabara ya Usagara-Kisesa KM 16.1 inayojengwa kwa kiwango cha lami ambapo ujenzi wake umefikia asilimia 75 na daraja la Nyashishi lenye urefu wa mita 67.9 ambalo ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 99.5 mkoani Mwanza.
Kwa upande wake, Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mwanza Eng. Marwa Rubirya, amesema ujenzi wa barabara hiyo unaendelea vizuri na mkandarasi atamaliza kwa wakati uliopangwa na viwango walivyokubaliana katika mkataba.
Ameongeza kuwa barabara hiyo inapita katika wilaya mbili ambazo ni Misungwi na Magu na kukamilika kwa barabara hiyo kutarahisisha huduma za usafirishaji wa abiria na mizigo katika wilaya hizo na mikoa jirani.
Labels:

Post a Comment

[facebook]

MKRdezign

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget